Social Icons

Sunday 25 May 2014

Tazama Come Back ya Real Madrid Dhidi ya Atletical UEFA,Diego Simeone Akiri Kujisikia Uchungu Baada Ya Kipigo


Kocha wa Atletico Madrid Diego Simeone amekiri kuwa anasikia uchungu baada Jana Usiku Mahasimu wao wakubwa Real Madrid kutwaa UEFA CHAMPIONZ LIGI walipotoka nyuma kwa Bao 1-0 na kushinda 4-1 kwenye Fainali iliyochezwa Mjini Lisbon, Ureno na kwenda hadi Dakika 120 baada ya Sare ya 1-1 katika Dakika 90.


Kikosi cha Simeone kilibakisha Sekunde tu kutwaa Ubingwa wa Ulaya walipokuwa wakiongoza Bao 1-0 na Dakika 90 kwisha lakini zikaongezwa Dakika 5 ambapo katika Dakika ya 3 yake Sergio Ramos akaisawazishia Real ambao walielekea kwenye ushindi baada ya kuongeza Bao 3 nyingine katika Dakika za Nyongeza 30 kwa Bao za Gareth Bale, Marcelo na Penati ya Cristiano Ronaldo.


Simeone amesema: “Sisikii huzuni ila nasikia uchungu kwamba hatukufikia malengo. Katika maisha, Siku moja una kila kitu, na nyingine huna chochote!”Huenda UEFA wakamchukulia hatua zaidi Diego Simeone kwani Dakika za mwishoni kabisa alivamia Uwanja na kwenda kumkabili Sentahafu wa Real Raphael Varane na Refa Bjorn Kuipers wa Holland akaamua kumtoa nje kwa Kadi Nyekundu.Hata hivyo, Simeone amesema anasikia fahari kwa Kikosi chake ambacho Wiki iliyopita kilitwaa Ubingwa wa Spain, La Liga, kwa mara ya kwanza tangu 1996.


Amesema: “Nimewaambia Wachezaji wangu wasilie. Wasikie fahari na kuufikiria Msimu ujao.”Alipohojiwa kuhusu kumwanzisha Diego Costa wakati alikuwa Majeruhi na matokeo yake alidumu Dakika 9 tu kwenye Mechi hiyo, Simeone alieleza: “Ilikuwa ni jukumu langu na ni wazi nilifanya kosa!”

Baada ya Miaka 12, Mameneja 11, na Mamilioni ya Fedha kuwekeza kwa Wachezaji wapya, ile ndoto ya Real Madrid ya 'La Decima', Taji la 10 Ulaya, Usiku huu imetimia huko Lisbon, Ureno, ndani ya Estadio Da Luz, baada kuichapa Atletico Madrid Bao 4-1 kwenye Fainali ya UEFA CHAMPIONZ LIGI iliyokwenda Dakika 120 baada kuwa 1-1 baada Dakika 90.

Usiku huu pia, Kocha wa Real, Carlo Ancelotti, ameweka Historia ya kutwaa Taji la 3 Ulaya kama Meneja na kuifikia Rekodi ya Meneja wa Liverpool, Bob Paisley, ambae pia ametwaa Mataji Matatu.Lakini kama si ushujaa wa Sergio Ramos, ndoto hii ya Real isingetimia kwani walikuwa wameshakufa Bao 1-0, Dakika 90 zilimalizika, na kwenye Dakika ya 3 ya Dakika 5 za Nyongeza, Ramos ndie alieisawazishia Real.

Fainali hii ilipoanza, kwenye Dakika za mwanzoni, Real ndio walionyesha wako juu na Atletico kupata pigo Dakika ya 9 tu baada ya Straika wao mahiri, Diego Costa, kulazimika kutoka na nafasi yake kuchukuliwa na Lopez.Hata hivyo, Atletico walionekana kuikamia sana Mechi hii na kutowapa nafasi Real kutuliza Mpira kiasi ambacho nafasi pekee kwa Real katika Kipindi cha Kwanza ilikuwa ni ya Gareth Bale ambae alipiga nje akiwa kwenye nafasi nzuri sana kufunga na mara baadae Real wakatoa Kona ya kipuuzi ambayo ilileta madhara makubwa kwao. 

Makosa makubwa ya Kipa Nambari Wani wa Spain, Iker Casillas, ndio yaliowapa Atletico Bao lao katika Dakika ya 36 baada kupigwa Kona na kuokolewa na Mpira kumkuta Diego Godin, Mchezaji kutoka Uruguay, aliepiga Kichwa kuurudisha Mpira Golini lakini wakati huo Casillas alikuwa keshatoka Golini na Kichwa hicho kumpita juu na licha ya juhudi zake kurudi mstarini na kuokoa hakufanikiwa.Diego Godin ndie aliewapa Atletico Ubingwa La Liga Wikiendi iliyopita baada Kichwa chake kuipa Bao la kusawazisha huko Nou Camp walipotoka 1-1 na Barcelona na Bao la Leo kwa Atletico ni Bao lake la 8 Msimu huu – na yote ni Kichwa.

Hadi Mapumziko Atletico walikuwa mbele kwa Bao 1-0.
Kipindi cha Pili Atletico walianza vyema lakini kadiri Dakika zikiendelea kuyoyoma Real ndio walikuja juu na hasa Dakika 20 za mwisho lakini umaliziaji mbovu, hasa Bale, na Difensi ngangali ya Atletico iliwazuia.
Baada Dakika 90 kumalizika na Bango kuashiria Dakika 5 za Nyongeza, kwenye Dakika ya 93, Kona ya Real iliunganishwa kwa Kichwa safi cha Sergio Ramos na kuipa Real Bao la kusawazisha na Mechi kwenda Dakika 30 za Nyongeza.

Hilo lilikuwa Bao la 6 kwa Ramos katika Mechi 7 zilizopita.
Nusu ya Kwanza ya Dakika za Nyongeza 30 haikuzaa Bao lolote.
Dakika ya 110, Angel Di Maria alikata mbuga toka kushoto na Shuti lake kuokolewa na Kipa Courtois na kumkuta Gareth Bale aliefunga kwa Kichwa na kuipa Real uongozi wa Bao 2-1.Dakika ya 117 Pasi ya Ronaldo ilimkuta Marcelo ambae alisonga mbele na kuachi Shuti la chini na Real kupiga Bao lao la 3.

Dakika ya 119, Ronaldo alifunga Bao la 4 kwa Penati baada ya yeye mwenyewe kuchezewa Rafu na Godin.
Hilo ni Bao la 17 kwa Ronaldo kwenye UEFA CHAMPIONZ LIGI Msimu hu…NI REKODI MPYA.
Hadi mwisho Real 4 Atletico 1, NDOTO YA ‘LA DECIMA’ IMETIMIA!

VIKOSI VINAVYOANZA:
REAL MADRID [Mfumo 4-3-3]:
Casillas, Carvajal, Varane, Sergio Ramos, Fabio Coentrao, Modric, Khedira, Di Maria, Bale, Benzema, Ronaldo.
Akiba: Diego Lopez, Pepe, Marcelo, Arbeloa, Morata, Isco, Illarramendi.
ATLETICO MADRID [Mfumo 4-4-2]:
Courtois, Juanfran, Miranda, Godin, Filipe Luis, Raul Garcia, Gabi, Tiago, Koke, Villa, Diego Costa
Akiba: Aranzubia, Mario Suarez, Adrian, Rodriguez, Alderweireld, Diego, Sosa.

Refa: Bjorn Kuipers [Holland]
Tazama hapa magoli na shangwe za Real madrid

No comments:

Post a Comment